MRADI WA
KUSWAHILISHA PROGRAMU HURIA
WARSHA YA ARUSHA
1-5 NOVEMBA 2004-11-22
MADA YA MAFUNZO
UKUZAJI WA
ISTILAHI: MISINGI YA KISARUFI
Zsm Mochiwa
1. UTANGULIZI
Kukua, kwa nafsi yake, ni
kuongezeka nguvu, kimo, ukubwa, umri, n.k. Inaposemwa kuwa, lugha fulani
inakua, ina maana inaongezeka uwezo wa kutekeleza majukumu yake; inapata nguvu
za kimawasiliano katika kuratili (articulate)
ulimwengu kwa usahihi zaidi.
Kukua kwa Kiswahili, kwa
mfano, huonekana kwa kuingia katika matumizi, maneno mapya au kutumika kwa
maneno makuukuu kwa maana mpya. Kwa kadri miaka inavyopita Kiswahili hutoka
katika kambi ya jumla jamala (generalities)
na kuzidi kuwa na umahususi (specificity).
Badala ya kuwa na neno moja, mguu,
kwa mfano, lenye maana ya sehemu ya mwili
kuanzia kiunoni hadi wayoni, kukua kwa Kiswahili kutaugawa mguu huo huo,
uwe na kiweo/paja, kiga, muundi, futi, chafu, n.k.
Kukua ni miongoni mwa nduni (features) za kimaumbile za kitu cho
chote kilicho hai. Kwa kuwa hai,
Kiswahili hupokea, kila uchao, maneno na/au vipengele mbali mbali vya lugha,
mwafaka wa mahitaji mapya yanayozuka.
Uwezo huu wa Kiswahili wa kujipanga upya kwa kulingana na changamoto
mpya, umo ndani ya maumbile yake.
Siri hii ya maumbile ya lugha huwa mwega wa kauli mbili
zinazotolewa mara kwa mara na wanaisimu (linguists). Wataalam hao wanadai kuwa, nafsi ya lugha
yoyote, imo katika sarufi yake. Hivi ni kusema, sarufi ndiyo inayoipa lugha ile
dhati yake, yaani, ile nidhamu ya kuunda maneno yake, kuyapangilia na kuyatamka.
Kwa kigezo hicho, Kiingereza, kwa mfano, ni mbali na Kiswahili.
Hiyo mosi, lakini pili, kwa kigezo hiki cha sarufi, hakuna lugha
yo yote iliyo ndogo au kubwa kuliko nyingine.
Kwa kigezo cha sarufi, Kiswahili na Kiingereza au lugha nyingine yoyote
ni sawa. Kinyume cha hivyo, itakuwa vigumu Kiingereza kupata nafsi ya lugha kwa
sababu, zaidi ya asilimia sabini ya maneno yake ni ya mkopo. Lakini kwa
kuingizwa kwa maneno hayo ya kigeni katika nidhamu maalum, yaani ile sarufi
yake, Kiingereza kimebakia na nafsi yake.
Maadam inakubalika kwamba
zinakua, basi si muhali hata kidogo, kudai kuwa lugha yoyote hai itakuwa na
mabadiliko kila uchao. Mabadiliko hayo
ndani ya maumbile ya lugha hutokea ama kwa polepole ama kinguvunguvu. Mabadiliko
ya polepole ndiyo yaliyo ya kawaida katika uhai wa lugha. Ni mabadiliko yanayoletwa na mtu mmoja mmoja
katika shughuli za kila siku.
Mtu mmoja, kwa mfano,
akigundua kitu kipya katika utafiti wake,
hukipatia jina. Linapoingia
kwa mara ya kwanza, jina lile huwa kipengele kipya cha msamiati. Katika
biashara yake, mfanya biashara huleta bidhaa mpya na majina yake ambayo
yatakuwa mapya katika lugha ya jumuia.
Mathalan, maneno redio au sukari au gari, yaliingia
katika Kiswahili kutoka katika Kiingereza kwa jinsi hiyo. Hata hivyo, kwa kuwa bidhaa hizi hazikuingia
kwa siku moja, ni dhahiri kuwa maneno haya nayo, hayakuingia kwa siku moja.
Maneno tunayoingiza katika Kiswahili hivi sasa kwa ajili ya
Uswahilishaji wa teknolojia ya kompyuta, ni mfano hai wa mabadiliko ya kinguvunguvu.
Tunataka Kiswahili kieleze kikamilifu teknolojia ya mawasiliano ya
Kompyuta. Tumepanga kuwa baada ya
kipindi cha miezi mitatu, Kiswahili kiwe na maneno ya teknolojia hiyo
yasiyopungua 1300.
Haya ni mabadiliko makubwa ambayo yatawapa changamoto
watumiaji. Kwa kuingia kwa muda mfupi
kama huu, watumiaji hulazimika kujifunza maneno mengi kwa wakati mmoja.
Kujifunza idadi kubwa ya maneno kama hii ni sawa na kujifunza upya, lugha
ambayo waliijua. Mabadiliko haya
huwanyang’anya wazungumzaji ule umilisi (competence)
wa lugha yao waliokuwa nao kabla ya zoezi hili.
Kutokana na kweli hii, zoezi
hili halina budi kufuata, kwa kadri itakavyowezekana, ruwaza (patterns) za
lugha yenyewe. Matumizi sahihi ya ruwaza za kifonolojia, kimofolojia,
kisintaksia, kisemantiki, n.k. ndiyo yatakayosababisha matunda ya zoezi hili
kupata mlahaka wa walengwa.
Litakapogagamiza mambo, zoezi hili linaweza kuleta athari za namna
nyingi, lakini hapa nitataja mbili.
Kwa upande mmoja, bidhaa zetu zinaweza zisinunulike. Hii ina maana
kuwa, walengwa wa zoezi letu wanaweza kuona uzito wa kupokea maneno
tutakayounda. Watakapoona ugeni ‘mnene’ wa kimatamshi au wa kimofolojia au wa
kisintaksia, watasema: hicho si Kiswahili! Kutozizingatia ruwaza hizi ni
kuwalazimisha walengwa wajifunze upya fonolojia, mofolojia, sintaksia ya lugha
yao wenyewe. Haya si mabadiliko yanayokubalika kwa urahisi.
Kwa upande mwingine zoezi hili linaweza kuingiza katika
Kiswahili, ulemavu utakaopunguza kiwango cha ujifunzikaji (learnability) wa lugha hii.
Mathalan, tukisha kubali kuvuruga ruwaza za umoja/uwingi, tukatia katoto/vitoto, tunaingiza ugeni
unaopunguza ujifunzikaji. Maana, mwega wa ujifunzikaji wa lugha yoyote ni zile
ruwaza za desturi zilizomo. Zitakapoingia ruwaza nyingine, tena kwa wingi, tatizo
la kupungua kwa ujifunzikaji na hata kukosa mlahaka (reception) huongezeka.
Tujipe fursa ya kuabiri baadhi ya ruwaza hizo ambazo hujenga misingi ya
kisarufi.
2. MISINGI YA KISARUFI
Kuizingatia misingi ya
kisarufi ya lugha kwa karibu katika jitihada ya kupanua msamiati ni kuikuza
lugha kwa kuitumia nafsi yake. Zinapotumika
ruwaza mbali mbali zilizomo
ndani yake, katika viwango mbali mbali vya
kifonolojia na kifonetiki, kimofolojia, kisintaksia na kisemantiki,
lugha hukua kwa mujibu wa maumbile yake.
Katika makala hii, tutaelezea ruwaza za kimofolojia kwa undani baada ya
kueleza kwa ufupi hizi ruwaza nyingine.
2.1
Kifonolojia na kifonetiki
Kimsingi, kila lugha ina
mpangilio wa desturi wa sauti na matamshi yake. Katika kiwango cha fonolojia, kuna mpangilio wa fonimu
uliokubalika. Kwa makusudi yetu hapa, tuchukue fonimu kuwa sauti ndogo ambazo
huwakilishwa na herufi hizi tunazotumia katika maandiko. Fonimu moja au mbili
huunda silabi, kama vile, a, ba, ta, ka, n.k.
Kila lugha hupangilia sauti zake kwa namna yake. Mathalan, silabi zifuatazo huonekana kwa wingi katika Kiswahili:
1. I mifano: au, ua, aua
KI
mifano: kata, tuta, na, mama, nani, nini
KKI mifano
ndondo,
mbumbumbu, ndumba
KKKI mifano: mbwanda, mbweu,
shindwa
Aidha, katika Kiswahili,
mfululizo wa KKKI hujengeka kwa sauti teule. Sauti ya kwanza katika silabi ya
KKKI huwa m au n, ya pili inakuwa b
ikiwa imeanza m au d au g
ikiwa ya kwanza ni n. Sauti ya tatu
itakuwa w. Kinyume cha utaratibu huu, silabi itakayotumia sauti nyingine
haina mlahaka katika Kiswahili.
Aidha, ingawa kwa kawaida
Kiswahili hutamkwa kwa jinsi kinavyoandikwa, lakini yako mazingira ambayo
yanaonesha kuwa fonimu huathiriana. Hali hii, inajitokeza katika maneno kama vile mwili, kwenda, twende n.k. Kwa msisitizo au kwa makusudi ya kuratili,
maneno haya hupata yakatamkwa muili, kuenda, tuende, n.k. Fikiria jinsi
unavyotamka maneno yafuatayo :
2. Mwambie (kwa haraka)
muambie (kwa
pole pole na kwa msisitizo)
kwenda (kwa haraka)
kuenda (kwa pole pole na
kwa msisitizo)
Jambo
la kukumbuka hapa ni kwamba, tunapounda neno, hatuna budi tukumbuke mpangilio
wa sauti pamoja na matamshi ya sauti hizo. Aidha, jambo hili ni muhimu zaidi
wakati wa kutohoa. Tunapotohoa neno la kigeni tunalipatia uenyeji wa matamshi
katika Kiswahili. Namna bora ya kutohoa neno, ni mtohoaji kujifanya kana kwamba
hajui ile lugha inayotoa neno linalotoholewa. Fikiria, microprocessor, kwa mfano, makorosesa
linafidi mradi ? Wewe ungelitohoaje ?
2.2 Kisintaksia
na Kisemantiki
Katika kiwango
cha sintaksia, Kiswahili kina mpangilio wa kutangaza kitu cha kusifiwa kabla ya
kukisifu. Mwenendo huu huenda kinyume
cha Kiingereza ambacho hupangilia sifa kwanza kabla ya kutaja kinachosifiwa. Tuangalie mifano hii:
3. Kiswahili : MTOTO mzuri, mweusi wa Kinyamwezi
Kiingereza :
A good, black Nyamwezi
CHILD.
2.3
Kimofolojia :
Katika
kiwango hiki, tunakutana na maumbo ya maneno. Karibu kila neno katika
Kiswahili, kama zilivyo lugha za Kibantu, lina sehemu zisizopungua mbili. Data
inayofuata, kwa mfano, ina maneno yenye sehemu mbili. Sehemu ya kwanza inataja idadi
na nyingine inadhihirisha dhati au nafsi ya kitu kinachotajwa na neno. Tuangalie maneno hayo :
4. M-toto WA-toto
KI-tabu VI-tabu
JI-we MA-we
Katika
mifano ya hapo juu, M- ina maana ya
mmoja, KI – ina maana ya kimoja na JI – ina maana ya moja. Hali kadhalika, ingawa kwa maumbo tofauti,
lakini, WA-, VI-, na MA huleta
maana ya ‘zaidi ya moja’. Baada ya
kutangaza idadi kwa maumbo ya herufi kubwa, sehemu ya kila neno iliyobakia,
yaani, -toto, -tabu, na -we hutangaza nafsi ya kitu chenye idadi
iliyotanguliwa kutajwa. Hivyo –toto ni child au children
kutegemea idadi inayotangazwa mwanzoni.
Kimofolojia muundo wa nomino za Kiswahili hudhihirisha ruwaza hii.
5.
IDADI
|
DHATI |
|
M |
Toto |
|
WA |
Toto |
|
KI |
Tabu |
|
VI |
Tabu |
|
JI |
We |
|
MA |
We |
Ruwaza hii si ya
Kiswahili pekee, bali pia, hudhihirika katika lugha nyingine, hususan za Kibantu.
Lakini ruwaza ya Kiingereza huenda kinyume cha hii ya Kiswahili kwa
kuanza na dhati na kumalizia idadi, kama mifano hii ilivyo:
6
DHATI
|
IDADI |
|
boy |
s |
|
cat |
s |
|
house |
s |
Wakati mwingine, tunapounda istilahi, haiwezekani kuzingatia kwa karibu mpangilio huo wa maumbo. Hii inajitokeza zaidi katika maneno ya sayansi za maumbile, kama vile, kemia, fizikia, n.k. Kwa mfano, tunapotohoa neno Carbondioxide, tunalazimika kuchukua mpangilio usio wa Kiswahili. Tuchukue kuwa tunatohoa Carbon kuwa Kaboni, di kuwa mbili au maradufu na oxygen kuwa oksijeni. Mpangilio huu, bila ya kubadilishwa unakifanya Kiswahili kipokee mpangilio mpya wa maumbo. Kwa kuwa ile di ni kiidadi cha oksijeni, kuchukua dioksaidi ni sawa na kuchukua mbili oksijeni badala ya oksijeni mbili.
Ingawa istilahi za kisayansi zina ‘ukimataifa fulani, lakini kila mkuzaji ana wajibu wa kulinda, kwa kadri iwezekanavyo, upekee wa lugha inayopokea istilahi zake. Mkuzaji hana budi kulinda ruwaza kwa maana ya kuzitumia katika mchakato wa ukuzaji. Faida kubwa ya jitihadi hizi ni kuzifanya itilahi hizo zikubalike na ya pili ni kulinda ufunzikaji wa lugha yenyewe. Yanapozidi, maneno yanayokiuka mikondo ya kimaumbile hupoteza sifa zote mbili: ya mlahaka wa maneno yenyewe na ujifunzikaji wa lugha inayohusika.
Uhai wa vitenzi
vya lugha za Kibantu unajitokeza katika michakato ya aina mbili. Kwa upande
mmoja vitenzi vya Kibantu hunyumbuka. Mzizi wa kitenzi cha Kibantu hupokea
maumbo yanayokifanya kiwe kirefu. Mzizi
wa piga ni pig. Mzizi pig unaponyumbuliwa hutupatia vitenzi mbali mbali kama
hivi:
7. piga,
pigana, pigia, pigiana, pigisha, pigishana, pigishania, n.k.
Vitenzi hivi
vinachanuza maana moja ya msingi. Lakini kila kitenzi kinatofautika kidogo
kimaana kutokana na kuongezeka kwa maumbo.Katika kunyumbuka kwake, pig
imeongezewa –a, an-a, -I-a, -I-an-a, -ish-a, n.k. Kila umbo lililoingezwa
limeandamana na mabadiliko ya maana. Mathalan, ingawa kitenzi pigana kinachukua maana ya piga lakini pigana inapangilia upya washiriki wa kitendo. Kitenzi pigana
kinatangaza watu wawili au zaidi wanaoshiriki kupiga, kila mmoja dhidi ya mwenziwe.
Kweli hii ya
kuongezeka kwa nguvu ya kimawasiliano kutokana na unyumbukaji wa vitenzi
inadhihirika vizuri kwa kuangalia maisha ya -i/e-. Kutokea kwa – i/e – katika
kitenzi piga kikapata sura ya pigia,
hutupatia nguvu ya kueleza maana nyingi:
8. pigia
(a) piga kwa ajili/niaba ya / dhidi ya mtu
mwingine
(b) tumia chombo X kwa
kutekelezea kitendo
(c) tumia sehemu Y katika kupiga
(d) piga X kwa sababu ya Y
Kinapofunguliwa kwa kutumia
umbo la unyumbulishi – i/e - kitenzi
kinapata uwezo wa kuhusisha watu au vitu katika utekelezaji wa kitendo cha
msingi piga. Pengine maana hizi mbalimbali zinaweza
kupangiliwa hivi kwa kutumia kitenzi kingine PIKA.
9. PIKIA: (i)
Pika
kwa ajili ya watoto Pikia watoto
(nani?)
(ii) Pika kwa kutumia kuni Pikia kuni (nini?)
(iii) Pika
ndani ya jiko = Pikia jikoni (wapi?)
(iv) Pika kwa sababu ya taabu = Pikia taabu (kisa)
Kinadharia, kila kitenzi
kina uwezo wa kuingia katika unyumbulikaji unaozaa vitenzi vipya . Vitenzi
hivyo huchanuza ruwaza mahsusi ya
maana. Kwa kuitumia ruwaza hii, mtu
anaweza kupata tafsiri za Kingereza hiki:
10. Cook for someone
Cook because of/as a result of being forced by someone.
Mchakato huu wa
unyumbulikaji hufungua pazia la kuzaliwa kwa nomino ambazo ni chanzo imara cha
maneno mapya. Mathalan, tuchukue
kitenzi kingine PENDA. Kwa
kunyumbulika kwake, kitenzi hutupatia:
11. PENDANA, PENDEA, PENDEKA,
PENDEKEA, PENDEKEZA,
PENDELEA, PENDEZA, PENDEZEA, PENDEZEANA, n.k.
Maneno haya yanayozaliwa
hutupatia mwega wa mchakato wa pili ambao tutauita unominishaji. Huu ni
mchakato unaotupatia nomino. Kinadharia, kila kitenzi kinachojitokeza kinaweza
kunominishwa hivi:
12. pendano, pendeo, pendeko, pendekeo, pendekezo,
pendeleo, pendezo, pendezeo, pendezeano, n.k.
Ninasema kinadharia kwa
sababu, si kila nomino inayoibuka ina matumizi hai. Nomino kama pendeo, pendeko, pendekeo, pendezo,
pendezeo, pengine, mpaka sasa yana uhai katika ulimwengu wa ushairi zaidi
kuliko kwingineko. Lakini jambo la
msingi ni kwamba hatuna sababu inayotuzuia tusiyaingize katika matumizi maneno
hayo yanayozaliwa.
Aidha, ili tufaidi utajiri
huu, inatubidi tuwe macho kuelewa vyema kiunzi cha kisemantiki (semantic frame) cha nomino hizi. Katika kulifafanua suala hili, hatuna budi
kuabiri baadhi ya vijenzi vya nomino.
Kwa makusudi hayo tuchunguze, bila ya kuvinyumbua, uhai wa vitenzi shinda, tuma, peta na panda.
13. shinda
-shindi, -shindaji, -shinde ______________
tuma ___ -tumaji, -tume _______________
peta
____
-petaji, -pete
-peto
pinda
-pindi, -pindaji, -pinde, -pindo
Vijenzi vinavyotuletea
mizizi ya nomino tuliyoiona hivi punde ni:
14. -I mfano mshindi
-E “
mshinde
- JI “ mpetaji
- O “ pindo
Kila kijenzi kina maana
mahsusi. Tuangalie kimoja kimoja:
2.3.1
KIJENZI
–I
Kijenzi -I hutuletea nomino kama vile: msomi,
mjenzi, mvuvi, n.k. Kila kinapotumika, kijenzi hiki hutangaza
utaalamu, uzoevu wa kujihusisha na tendo linalofungamana na kitenzi. Msomi, kwa mfano, ni mtu aliyesoma jambo
fulani kwa undani, mtaalamu mzoevu wa uwanja wa taaluma fulani. Hali kadhalika, mvuvi ni mzoevu, mtaalam wa
kuvua; hupata riziki zake kwa kazi hiyo. Hivyo nomino nyingi za Kiingereza
zinazodokeza professionalism n.k.
huweza kufasiriwa kwa nomino zenye kijenzi hiki.
15. Fisherman mvuvi
(vua)
builder/constructor mjenzi (jenga)
Orator msemi (sema)
Lover mpenzi
(penda)
Cook mpishi (pika)
Hunter msasi
(saka)
Kijenzi hiki kinajitokeza
katika vitenzi ambavyo hutumika pamoja na maneno mengine yanayotaja vitu, watu,
n.k. Mifano hai ya vitenzi hivyo
ni: pika ugali. suka nywele,
penda watu, n.k. Vitenzi vya aina hii ndivyo vinavyotuletea nomino hizi
zifuatazo:
16. Mpishi (wa ugali), yaani,
mtu anayepika ugali
Msusi (wa nywele), yaani, mtu
anayesuka nywele
Mpenzi (wa watu), yaani, mtu
anayependa watu kwa dhati.
Nomino hizi kwa pamoja
hutangaza ‘watenzi’ wa mambo. Mpenzi, kwa mfano hapendwi bali
anapenda! Mtu anapodai kuwa fulani ni mpenzi
wake ana maana kuwa huyo fulani ndiye anayempenda. Hivyo ni kusema, mtu
huyo ni mpendwa wa huyo fulani ambaye ni mpenzi
wake. Sasa tuangalie kijenzi –ji
ambacho ki karibu na hiki tulichoona hivi punde.
2.3.2 Kijenzi
–ji
Kijenzi hiki pia hutangaza
‘watenzi’ wa aina fulani. Tofauti kati ya kijenzi hiki na kile kingine imo
katika uwezo, uzoevu, utaalamu, ung’ang’anizi, n.k. Mvuaji si mvuvi wa kila
siku; mjengaji si mjenzi wa kila siku. Wote hawa huvua na kujenga kwa siku moja moja. Kwa kawaida, watu hawa hawapati riziki zao
za kila siku kwa njia ya kuvua wala kujenga.
Katika kujenga, kwa mfano, mjenzi ana utaalam wa hakika pamoja na
uzoevu na si ajabu ana vyeti kabisa. Aidha, anaponyang’anywa tenda za kujenga,
si ajabu akawa amepoteza hata mzungu wa maisha yake kabisa. Mjengaji ni mtu wa
kubabiababia tu. Hategemei kazi hiyo hyo tu. Yeye, aghalabu ya mambo ni mtu wa
‘kubangaiza’. Tuangalie mifano hii michache:
17. Vuna Mvunaji (ling. na mvuni)
Choma Mchomaji
(ling. na mchomi)
Chunga Mchungaji
(ling. na mchungi)
Tenda Mtendaji (ling. na Mtenzi)
Kijenzi –ji kimestawi zaidi, pengine kuliko
–I. Hali hii inaashiria kuwa utenzi wa mambo ni wa nadra zaidi ya utendaji.
Watu wengi hufanya mambo kwa kupitia kuliko kuishia. Hata hivyo, inafaa ikumbukwe hapa kwamba, kijenzi –ji hupata kikapewa hadhi sawa na kile
cha –i. Mathalan, Mwenyekiti Mtendaji wa Shirika fulani,
si wa siku moja moja; ni mtenzi hasa. Aidha, sahihi ya mambo ingekuwa aitwe Mwenyekiti Mtenzi! Tuabiri kijenzi –0
2.3.3.
Kijenzi –O
Karibu vitenzi vyote
hukitumia kijenzi hiki kwa kuzalia nomino zinazotangaza maana mbalimbali.
Miongoni mwa maana hizi ni ile ya kile kinachotokea baada ya utenzi. Hii ina
maana kuwa, ile nomino inayozaliwa inasema tunda la kitenzi chake. Tuangalie
vitenzi vichache ili tulithibitishe dai hili:
18. Ziba zibo: kitu
kinachotumika katika mradi wa kuziba
Futa futo: kitu kinachotumika katika mradi wa kufuta
Pata pato: kitu ambacho mtu anapata
Zaa zao: kitu ambacho kinazaliwa
Peta peto: kitu kinachopatikana baada ya kupeta
Kila nomino ambayo ina
kijenzi cha –O hutangaza moja kati ya
mambo mawili. Ama inatangaza tunda.
Mfano mmoja wa maana hiyo ni pato
ambalo ni tunda la kupata. Pato
hutangaza kupata kwenyewe. Maana hii inajitokeza pia katika maana ya zao. Zao
ni tunda la kitendo cha kuzaa.
Wakati mwingine, nomino
zinaweza kutangaza vifaa vya utekelezaji wa vitendo vinavyohusika. Tuchukue
mfano wa kiZIBO. Kizibo ni kitu cha kutumia katika kuziba. Viko vitenzi vingi vyenye uwezo wa kuzaa nomino za aina
hii. Tuangalie vitenzi hivi:
19. Unda Nyundo kitu kinachotumika katika kuunda
Tega Mtego kitu cha kutumia kwa ajili ya kutega
Kaga Kago kitu
kinachokaga
Finga Fingo kitu kinachotumika kwa ajili ya
kufinga
Kijenzi –O kinaweza
kutangaza namna kitenzi kinavyoingizwa katika tendo. Maana ya mpigo, nomino inayotokana na kitenzi
PIGA ni namna ya kupiga. Nguvu za kimawasiliano za kijenzi hiki hudhihirika
hivi:
20. mpigo namna ya kupiga
mapigo dharuba
(marudio ya) za kupiga
kipigo kitendo
cha kupigwa
Mzibo namna
ya kuziba
Kizibo kifaa
kinachoziba
Mfuto namna
ya kufuta
Mfuto kitu
cha kinachofuta
Kwa matumizi
ya maombo mbali mbali ya idadi, inawezekana kutumia shina moja lanomino kama
pigo kupata nomino zaidi ya moja. Mfano mzuri ni ule tulioona wa mpigo, mapigo
na kipigo. Kila mjenzi wa istilahi aliye na hazina ya namna hii ya misingi ya
kimofolojia atakuwa anaingiza maneno ambayo hayagunwi na walengwa. Aidha,
maneno hayo huweza kupokewa bila ya kusita. Tuangalie kijenzi cha mwisho.
2.3.4
Kijenzi
–E
Msingi wa
kimaana wa kijenzi hiki hutaja kitu ‘kinachotenzwa’. Hapa pana mifano dhahiri:
21. Mtume mtu
aliyetumwa
Upinde uliopindwa
Upote uliopotwa
Pete iliyopetwa
Kiumbe kilichoumbwa
MWISHO.
Tulichoshughulikia
kwa juu juu hapa ni michakato ya aina mbili. Kwanza, kuna mchakato ambao unazaa
vitenzi kutokana na kunyumbuka kwa vitenzi vyenyewe. Pili, tumeonesha mchakato
mwingine ambao hutupatia nomino. Kinadharia, vile vitenzi vinavyozaliwa katika
mchakato wa kwanza, vinaweza kutumia vijenzi vilivyojadiliwa vikazaa nomino. Michakato
miwili hii, inaweza kuelelezwa hivi:
![]()
![]()
![]()
![]()
![]()
![]()
![]()
e *
* * *
* *
*
ji * * * * * * *
i * * * * * *
*
o * * * * * *
*
Pend ea eka
ekea ekeza elea eza ezeana
Matumizi ya misingi ya kisarufi katika ukuzaji wa istilahi
husaidia kwa namna mbili. Kwa upande mmoja, misingi hii huongeza mlahaka wa
maneno yanayozaliwa. Kwa upande mwingine, misingi hii hukipatia Kiswahili
ukuaji wa kimaumbile.